23 Paulo akawakazia macho wajumbe wa baraza, akasema, “Ndugu zangu, mimi nimeishi nikiwa na dhamiri safi kabisa siku zote mbele za Mungu, mpaka leo.” Kuhani mkuu Anania akaamuru wale waliokuwa karibu na Paulo wampige kofi mdomoni. Ndipo Paulo akasema, “Mungu atakupiga, wewe ukuta uliopakwa chokaa! Unawe zaje kusikiliza kesi hii kwa mujibu wa sheria, na hapo hapo, kinyume cha sheria, unaamuru nipigwe?” Wale watu waliokuwa wamesimama karibu wakamwambia Paulo, “Mbona unamtukana kuhani mkuu wa Mungu?” Paulo akajibu, “Ndugu zangu, sikujua kwamba yeye ni kuhani mkuu. Kwa maana Maandiko yanasema, ‘Usimseme vibaya kiongozi wa watu wako.’ ” Paulo alipotambua ya kuwa baadhi ya wajumbe wa baraza walikuwa Masadukayo na wengine ni Mafarisayo alisema nao kwa sauti kubwa, “Ndugu zangu! Mimi ni Mfarisayo, mtoto wa Mafarisayo; na hapa nimeshitakiwa kuhusu tumaini juu ya ufufuo wa wafu.” Aliposema haya, Mafarisayo na Masadukayo wakafarakana na baraza zima likagawanyika. Kwa maana Masadukayo wanaamini kwamba hakuna ufufuo, wala hakuna malaika au roho; lakini Mafarisayo wanaamini haya yote. Kelele zikazidi sana; na baadhi ya waandishi wa sheria wa upande wa Mafarisayo, wakasimama wakiwapinga wengine wakasema, “Hatuoni kosa lo lote alilofanya mtu huyu! Huenda ikawa malaika au roho amezungumza naye kweli!” 10 Mabishano yalipozidi kuwa makali, yule jemadari aliogopa kuwa wangeweza kumrarua Paulo vipande vipande. Kwa hiyo akaamuru askari wakamtoe Paulo alipokuwa, arudishwe kwenye ngome ya jeshi. 11 Usiku uliofuata, Bwana akamtokea Paulo akasimama karibu naye akamwambia, “Jipe moyo! Kama ulivyonishuhudia hapa Yerusalemu, itakubidi unishuhudie na huko Rumi pia.”

Njama Za Wayahudi Kumwua Paulo

12 Kulipopambazuka Wayahudi wakala njama ya kumwua Paulo. Wakaweka nadhiri kwamba hawatakula wala kunywa mpaka wamemwua Paulo. 13 Waliofanya mpango huu walikuwa zaidi ya watu arobaini. 14 Wakaenda kwa kuhani mkuu na wazee wakasema, “Tumeweka nad hiri ya pamoja kwamba hatutakula wala kunywa mpaka tumwue Paulo. 15 Kwa hiyo ninyi pamoja na baraza, pelekeni ombi kwa jemadari ili Paulo aletwe barazani, mtoe udhuru kwamba mnataka kuchunguza kesi yake kwa usahihi zaidi. Sisi tutakuwa tayari kumwua hata kabla hajakaribia kufika hapa.” 16 Basi kumbe binamu yake Paulo alisikia kuhusu mpango huu. Akaenda katika ngome ya jeshi akamweleza Paulo mambo haya. 17 Paulo akamwita mmoja wa wale maaskari akamwambia, “Mchukue kijana huyu kwa jemadari, ana neno la kumwambia.” 18 Yule askari akamchukua yule kijana mpaka kwa jemadari akamwambia, “Yule mfungwa Paulo aliniita akaniambia nimlete huyu kijana kwako, kwa sababu ana neno la kukuambia.” 19 Yule jemadari akamchukua yule kijana kando akamwuliza, “Unataka kuniambia nini?” 20 Naye akasema, “Wayahudi wameku baliana wakuombe kesho umpeleke Paulo kwenye Baraza lao kwa kisingizio kwamba wanataka kuchunguza kesi yake kwa uangalifu zaidi. 21 Lakini usikubali ombi lao kwa maana zaidi ya watu aro baini wamekula njama kwamba hawatakula wala kunywa mpaka wamwue Paulo nao wamejiweka tayari kumvizia ukishakubali ombi lao.” 22 Yule jemadari akamruhusu yule kijana aende, akamwonya akisema, “Usimwambie mtu ye yote kwamba umenieleza habari hizi.”

Paulo Apelekwa Kaisaria Kwa Gavana Feliksi

23 Yule jemadari akawaita maaskari wawili akawaambia, “Tay arisheni askari mia mbili watakaokwenda Kaisaria pamoja na askari wa farasi sabini, na askari wa mikuki mia mbili; nanyi muwe tay ari kuondoka leo saa tatu za usiku. 24 Pia tayarisheni na farasi watakaotumiwa na Paulo, mumpeleke salama mpaka kwa gavana Feliksi.” 25 Kisha akaandika barua kwa Feliksi kama ifuatavyo: 26 “Mimi Klaudio Lisia, nakuandikia wewe gavana mtukufu Feliksi. Salamu. 27 Mtu huyu alikamatwa na Wayahudi wakawa kar ibu kumwua, ndipo mimi nilipofika na askari wangu nikamwokoa kwa kuwa nilipata habari kwamba yeye ni raia wa Kirumi. 28 Nami nikampeleka mbele ya baraza lao ili nipate kujua kosa alilofanya. 29 Ndipo nikagundua ya kuwa alikuwa anashtakiwa kuhusu sheria yao, lakini hakuwa na kosa la kustahili kifo au kifungo. 30 Lakini nilipata habari kwamba kuna mpango wa kumwua nikaamua nimpeleke kwako mara moja, nikawaamuru washitaki wake walete mashtaka yao kwako.” 31 Basi wale askari wakamchukua Paulo usiku wakampeleka mpaka Antipatri kama walivyoamriwa. 32 Kesho yake wakarudi kituoni wakawaacha wale askari wa mikuki waendelee na safari pamoja na Paulo. 33 Walipofika Kaisaria walimpa Liwali ile barua na pia wakamkabidhi Paulo kwake. 34 Alipokwisha soma ile barua, alimwuliza Paulo ametoka jimbo gani. Alipofahamishwa kuwa anatoka Kilikia 35 alisema, “Nitasikiliza kesi yako mara tu washtaki wako watakapofika.” Akaamuru Paulo awekwe chini ya ulinzi katika ikulu ya Herode.

23 Paulo aliwatazama wajumbe wa baraza na kusema, “Ndugu zangu, Nimeishi maisha yangu katika njia nzuri mbele za Mungu. Daima nimefanya yale niliyodhani ni haki.” Anania,[a] kuhani mkuu alikuwa pale. Aliposikia hili, aliwaambia watu waliokuwa wamesisima karibu na Paulo wampige kwenye mdomo. Paulo akamwambia Anania, “Mungu atakupiga wewe pia! Wewe ni kama ukuta mchafu uliopakwa rangi nyeupe. Umeketi hapa na kunihukumu, ukitumia Sheria ya Musa. Lakini unawaambia wanipige wakati ni kinyume cha sheria.”

Watu waliokuwa wamesimama karibu na Paulo wakamwambia, “Una uhakika unataka kumtukana kuhani mkuu wa Mungu namna hiyo?”

Paulo akasema, “Ndugu zangu, sikufahamu kuwa mtu huyu ni kuhani mkuu. Maandiko yanasema, ‘Usiseme mambo mabaya kuhusu kiongozi wa watu wako.’”(A)

Paulo alijua kuwa baadhi ya watu kwenye baraza lile ni Masadukayo na baadhi yao ni Mafarisayo. Hivyo akapaza sauti akasema, “Ndugu zangu, Mimi ni Farisayo na baba yangu ni Farisayo! Nimeshitakiwa hapa kwa sababu ninaamini kuwa watu watafufuka kutoka kwa wafu.”

Paulo alipolisema hili, mabishano makubwa yakaanza kati ya Mafarisayo na Masadukayo. Baraza likagawanyika. (Masadukayo hawaamini katika ufufuo, malaika au roho. Lakini Mafarisayo wanaamini vyote.) Wayahudi hawa wote wakaanza kubishana kwa kupaza sauti. Baadhi ya walimu wa sheria, waliokuwa Mafarisayo wakasimama na kusema, “Hatuoni kosa lolote kwa mtu huyu. Inawezekana kwa hakika malaika au roho alizungumza naye.”

10 Mabishano yaligeuka kuwa mapigano na kamanda aliogopa kwamba Wayahudi wangempasua Paulo vipande vipande. Hivyo akawaambia askari wateremke, wamwondoe Paulo na kumweka mbali na Wayahudi hao katika jengo la jeshi.

11 Usiku uliofuata Bwana Yesu akaja na kusimama pembeni mwa Paulo. Akamwambia, “Uwe jasiri! Umewaambia watu kuhusu mimi humu Yerusalemu. Ni lazima ufanye vivyo hivyo Rumi.”

Baadhi ya Wayahudi Wapanga Kumwua Paulo

12 Asubuhi iliyofuata baadhi ya Wayahudi walifanya mpango wa kumwua Paulo. Walijiapiza kuwa hawatakula wala kunywa kitu chochote mpaka watakapomwua Paulo. 13 Walikuwa watu zaidi ya 40 waliofanya mpango huu. 14 Walikwenda wakaongea na viongozi wa makuhani na viongozi wa wazee wa Wayahudi. Walisema, “Tumejiwekea nadhiri kwamba hatutakula wala kunywa mpaka tumemwua Paulo. 15 Tunataka mfanye hivi: Mtumieni kamanda ujumbe kutoka kwenu na baraza kuu. Mwambieni mnamtaka amlete Paulo kwenu. Semeni kwamba mnataka kumwuliza maswali zaidi, tutamwua akiwa njiani kuja hapa.”

16 Lakini mpwaye Paulo aliusikia mpango huu. Alikwenda kwenye jengo la jeshi na kumwambia Paulo. 17 Kisha Paulo akamwita mmoja wa maofisa wa jeshi na kumwambia, “Mchukue huyu kijana kwa kamanda. Ana ujumbe kwa ajili yake.” 18 Hivyo ofisa wa jeshi akampeleka mpwaye Paulo kwa kamanda. Ofisa wa jeshi akasema, “Mfungwa Paulo ameniomba nimlete kijana huyu kwako. Ana kitu cha kukueleza.”

19 Kamanda akamchukua kijana na kwenda naye mahali ambapo wangekuwa peke yao. Kamanda akamwuliza, “Unataka kuniambia nini?”

20 Kijana akasema, “Baadhi ya Wayahudi wameamua kukuomba umpeleke Paulo kwenye mkutano wa baraza lao kesho. Wanataka wewe udhani kuwa wamepanga kumwuliza Paulo maswali zaidi. 21 Lakini usiwaamini! Zaidi ya watu 40 miongoni mwao wamejificha na wanasubiri kumwua. Wote wameweka nadhiri kuwa hawatakula wala kunywa mpaka wamemwua Paulo. Sasa hivi wanasubiri wewe ukubali.”

22 Kamanda akamtoa kijana, akamwambia, “Usimwambie yeyote kuwa umeniambia kuhusu mpango wao.”

Paulo Apelekwa Kaisaria

23 Ndipo Kamanda akawaita maofisa wawili wa jeshi. Akawaambia, “Ninataka baadhi ya watu kwenda Kaisaria. Andaeni askari mia mbili. Pia andaeni askari sabini waendao kwa farasi na mia mbili wa kubeba mikuki. Iweni tayari kuondoka saa tatu usiku. 24 Andaeni baadhi ya farasi kwa ajili ya Paulo kuendesha ili aweze kupelekwa kwa Gavana Feliki salama.” 25 Kamanda aliandika barua kuhusu Paulo. Hivi ndivyo alivyosema:

26 Kutoka kwa Klaudio Lisiasi.

Kwenda kwa Mheshimiwa Gavana Feliki.

Salamu:

27 Baadhi ya Wayahudi walimkamata mtu huyu na walikuwa karibu ya kumwua. Lakini nilipogundua kuwa ni raia wa Rumi, nilikwenda pamoja na askari wangu tukamwokoa. 28 Nilitaka kufahamu kwa nini walikuwa wanamshitaki. Hivyo nikampeleka kwenye mkutano wa baraza lao. 29 Hivi ndivyo nilivyoona: Wayahudi walisema mtu huyu alifanya mambo mabaya. Lakini mashitaka haya yalihusu sheria zao za Kiyahudi, na hakukuwa kosa lolote linaloweza kusababisha kufungwa au kifo. 30 Nimeambiwa kuwa baadhi ya Wayahudi walikuwa wanafanya mpango wa kumwua. Hivyo nimeamua kumleta kwako. Pia nimewaambia Wayahudi hao wakwambie walichonacho dhidi yake.

31 Askari walifanya kile walichoambiwa. Walimchukua Paulo na kumpeleka kwenye mji wa Antipatri usiku ule. 32 Siku iliyofuata askari wa farasi walikwenda na Paulo mpaka Kaisaria, lakini askari wengine na wale wa mikuki walirudi kwenye jengo la jeshi mjini Yerusalemu. 33 Askari wa farasi waliingia Kaisaria, wakampa barua Gavana Feliki, kisha wakamkabidhi Paulo kwake.

34 Gavana akaisoma barua na kumwuliza Paulo, “Unatoka jimbo gani?” Gavana alitambua kuwa Paulo alikuwa anatoka Kilikia. 35 Gavana akasema, “Nitakusikiliza Wayahudi wanaokushitaki watakapokuja hapa pia.” Kisha gavana akaamuru Paulo awekwe kwenye jumba la kifalme. (Jengo hili lilijengwa na Herode.)

Footnotes

  1. 23:2 Anania Si Anania anayetajwa katika Mdo 22:12.